Meneja Miradi wa Benki ya Absa, Bi. Munira Chambuso
akizungumza katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi
Tanzania (TPSF) kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, ikihuhusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam mwishoni
mwa wiki.
Benki ya Absa Tanzania kwa
kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), wameandaa semina
wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, kutoka sekta mbalimbali ili
kuwajengea uwezo katika elimu ya masuala ya kifedha pamoja na usimamizi wa uwekezaji, iliyofanyika jijini
Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa
Wanachama wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Bi. Kinanasy Seif alisema,
shirikisho hilo litaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuwawezesha
wanawake wajasiriamali kupitia programu za mafunzo na elimu zinazolenga kukuza
biashara na kuimarisha uchumi wao.
Alisema TPSF imekuwa ikitekeleza
programu mbalimbali za kuwawezesha wanawake katika nyanja tofauti za kibiashara
huku ikitambua mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya sekta binafsi na
uchumi wa taifa kwa ujumla.
“Tumefanikiwa kuwaleta pamoja
wanawake wajasiriamali kutoka maeneo mbalimbali ili wapate mafunzo ya elimu ya
fedha na uwekezaji kutoka Benki ya Absa, tunaamini maarifa haya yatawasaidia
kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kukuza biashara zao,” alisema Bi. Kinanasy
akiongeza kuwa ushirikiano kati ya TPSF na Benki ya Absa ni hatua muhimu katika
kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kujengewa uwezo na kufikia maendeleo
endelevu katika shughuli zao za kiuchumi.
Naye Ofisa Elimu kwa Mlipa Kodi
na Mawasiliano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutoka Mkoa wa Kodi wa
Kinondoni, Bw. Zephania Mange, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria za kodi
katika kujenga biashara imara na endelevu pamoja umuhimu wa walipakodi kutekeleza wajibu wao, na pia
kufahamu haki zao wanazostahili kupata kutoka katika mamlaka hiyo.
Alisema miongoni mwa haki hizo ni
usiri wa taarifa za kikodi, ambapo taarifa zote zinazowasilishwa na mlipakodi
zinapaswa kubaki siri na haziwezi kutolewa kwa watu wasiohusika. Aidha,
walipakodi wote wanapaswa kuhudumiwa kwa usawa bila upendeleo wowote.
“Walipakodi pia wana haki ya
kupinga maamuzi yanayotolewa na maafisa wa kodi pale wanapoona hawajaridhika
nayo kwani maamuzi ya awali sio ya mwisho, hivyo kuna fursa ya kukata rufaa kwa
kufuata taratibu zilizowekwa”, alisema Bw. Mange.
Kwa upande wa wajibu wa mlipa
kodi, ofisa huyo alisema mamlaka hiyo inawakumbusha
wafanyabiashara kuhakikisha wanajisajili kupata namba ya mlipa kodi (TIN) ndani
ya siku tano tangu waanze biashara, na pia wafanyabiashara wanaofikia mauzo
yanayostahili kwa mujibu wa sheria wanapaswa kutumia mashine za kutolea risiti
za kielektroniki (EFD) ama kujisajili kwenye mfumo wa Kodi ya Ongezeko la
Thamani (VAT) kwa waliokidhi vigezo.






No comments:
Post a Comment